Thursday 27 February 2014

Maambukizi Yanayosambazwa kwa Kujamiana (MYKK)


Tunaelezea kwenye safu hii maambukizi yanayosambazwa kwa kujamiana. Wasomaji wengi wamezoea kuyaita magonjwa ya zinaa lakini habari hii inataka tubadilishe tuyaite ‘Maambukizi Yanayosambazwa kwa Kujamiana (MYKK)’ na tutaelezea kwa nini.
 Wanaojua Kizungu labda watakumbuka kuwa hapo awali tulikuwa tunaita hali hizi ‘Sexually Transmitted Diseases (STD). Ukitafsiri moja kwa moja maana yake ni Magonjwa Yanayoambukizwa Kujamiana . Tuliacha kuyaita STD na sasa tunayaita ‘Sexually Transmitted Infections’ (STI) yaani Maambukizi Yanayosambazwa kwa Kujamiana.
Kuna tofauti kati ya magonjwa (diseases) na maambukizi (infections) kwa kuwa magonjwa mengine yanasababishwa na maambukizi. Kwa hiyo tofauti kati ya magonjwa na maambukizi ni kuwa maambukizi yanazaa magonjwa. (Tofauti kati ya yai na kuku ni kwamba kuku anataga  yai).
‘Sexually Transmitted Infection’ (STI)  kwa Kiswahili cha moja kwa moja ni Maambukizi Yanayosambazwa kwa Kujamiana. Sexually transmitted Diseases (STD)  ni Magonjwa Yanayoambukizwa kwa Kujamiana. Utaona kuwa hapa  kuna tofauti kati ya magonjwa (diseases) na maambukizi (infections) Tatizo hapa siyo la ugonjwa tu bali ni la maambukizi. Kunaweza kukawa na maambukizi yanayotokana na  kujamiana ambayo unayaona  maambukizi yenyewe, yaani unaona wadudu ambao mtu ameambukizwa kwa kujamiana, lakini huoni ugonjwa wenyewe. Hii inatokea wa mfano mtu anapoambukizwa na chawa wakati wa kujamiana  (chawa wa mafuzi). Unawaona chawa wenyewe lakini huoni ugonjwa.
Kwenye  tatizo la UKIMWI mtu anaambukizwa  na VVU. Haya ni maambukizi. Ugonjwa hauonekani moja ka moja bali kinachoonekana ni syndroma (dalili nyingi nyingi) inayosababishwa na magonjwa tegemezi yanayouvamia mwili baada ya kinga ya mwili kupungua. Maambukizi mengine kwa mfano ya kisonono na kaswende; ugonjwa unaonekana. Kwa sababu hizi za kuwa kuna hali nyingine ambapo ugonjwa hauonekani moja kwa moja na kwa kuwa katika hali zote kuna maambukizi basi ikakubalika hali hizi ziitwe Maambukizi Yanayosambazwa kwa Kujamiana (Sexually Transimitted Infections - STI)  Magonjwa Yanayosambazwa kwa Kujamiana (Sexually Transimitted  Diseases - STD)
Ni  Maambukizi ya Sinaa (MYS) au ni Maambukizi Yanayosambazwa kwa Kujamiana (MYKK)?
Ni lazima tuwashukuru wataalamu wanaojitahidi kutafsiri maneno yetu ya kisayansi kuyaweka kwenye lugha ya Kiswahili. Tushukuru kuwa tafsiri zao nyingi ni sawa na rahisi kuzitumia lakini kuna tafsiri ambazo wao wametupa kianzio ili na sisi tufikirie tuone kama zinahitaji kuboreshwa. Moja ya tafsiri ambayo inahitaji kuboreshwa ni hii ya kuziita hali hizi magonjwa. Tumeishatoa sababu hapo juu na kuelezea kuwa tuziite hali hizi maambukizi na siyo magonjwa.
Ukimwi unamtesa sana mwathirika
Kwa hiyo tuseme ni Maambukizi ya Sinaa?  Sinaa linamaanyisha starehe. Ni kama tunasema kuwa Maambukizi Yanayosambazwa kwa Kujamiana yanatokana na  sinaa, yanatokana na starehe. Hapa tunakuwa kama tunasema kuwa haya ni maambukizi yanatokana na kustarehe bila hata kusema ni starehe gani - ya kunywa pombe, ya kutumia madawa ya kulevya, ya kucheza dansi na musiki - starehe zipo nyingi. Tuyaite Maambukizi Yanayosambazwa na Starehe ya Kujamiana?
Ni ukweli kuwa ukichukulia kujamiana kama starehe utapata Maambukizi Yanayosambazwa kwa Kujamiana. Yanapotokea kati ya wanandoa yanatokana na mwanandoa mmoja au wote wawili kutokuwa waaminifu na kuchukulia kujamiiana kama starehe.
Ni vizuri jina la hali inayohusiana na ugonjwa unapolisikia linakueleza mengi juu ya hali yenyewe na linakuambia hata namna ya kujikinga na hali hiyo. Hapa ukisikia maneno matatu ya jina la hali hii ‘Maambukizi Yanayoambukizwa kwa  Kujamiana’ tayari umeishajua kuwa haya ni maambukizi; kuwa mwenzako anakuambukiza au wewe unamwambukiza. Ukisikia yanayosambazwa unajua kuwa yanasambazwa na siyo kwamba yanaambukizwa tu. Ukisema yanasambazwa tayari umeishasema kuwa yanaenea haraka sana kutoka mtu  hadi mtu. Ukisikia kuwa maambukizi haya yanatokana na kujamiana unaanza kujisemea ‘nijichunge sana na kujamiana ovyo ovyo.’
Maambukizi Yanayosambazwa kwa Kujamiana (MYKK) ni mtu kwa  mtu;  yaani yanatoka kwa mtu  mmoja yanaenda kwa mtu mwingine.  Siyo kama ilivyo kwenye ugonjwa wa kwa mfano malaria ambao vijidudu hutoka kwa mtu mmoja; vinaingia kwa mbu na baadaye kwa binadamu. Siyo kama wa kichocho ambao vijidudu vinatoka kwa mtu vinaingia kwenye konokono na baadaye vinaingia kwa mtu tena. Wataalamu wanaita hali hii ya jinsi vijidudu vinatoka kwa mwanadamu na baadaye kumrudia tena ‘mzunguko wa maambukizi’ ambapo kuna hatua mbali mbali.
Kwanza kuna wadudu wenyewe kwa mfano wanaosababisha Maambukizi Yanayosambazwa kwa Kujamiana; kuna hifadhi ya hao wadudu kwa mfano hapa anayewahifadhi ni binadamu; halafu wadudu wanaingia kwa mtu mwingine na huyo mtu mwingine anawapeleka tena kwa mtu mwingine. Maambukizi Yanayosambazwa kwa Kujamiana ni ya moja kwa moja kutoka kwa mtu hadi kwa mtu mwingine. Maambukizi ya magonjwa mengine yana mzunguko mrefu zaidi ambapo kuna wadudu wa maambukizi, kuna hifadhi yao ambayo moja inaweza ikawa binadamu (malaria na kichocho) au mnyama (kichaa cha mbwa); wadudu wanatoka kwenye hifadhi wanaingia kwenye mnyama mwingine kama kwa mfano kichocho kinaingia kwenye konokono, kinatoka huko na kuingia kwa binadamu. Kwa kujua mzunguko huu wa vijidudu vya magonjwa inajulikana ni wapi tuingilie ili kuuthibiti ugonjwa wenyewe. Kwa kuwa inajulikana kuwa mzunguko wa Maambukizi Yanayosambazwa kwa Kujamiana ni mtu kwenda kwa mtu; na yanaambukiza kwa kujamiana, kuyakinga haya maambukizi kunahusu kuiangalia hali ya kujamiana na kuhakikisha mtu anajamiana na mwenzake ambaye hana uwezekano wa kuwa na hifadhi ya Maambukizi Yanayosambazwa kwa Kujamiana (MYKK). Kuna watu ambao wana uwezekano zaidi wa kuwa hifadhi ya wadudu wa MYKK.  Kujikinga na maambukizi haya ni vema kutojamiana nao. Hawa ni watu wanaojamiana na watu wengi kwa mfano malaya au hata watu wa kawaida tu mradi wewe mwenyewe umemwangalia na kujua tabia yake. Ukishajua kuwa huyu anajamiana na wanaume au wanawake wengi au zaidi ya mmoja unajua kuna uwezekano kuwa yeye ni hifadhi ya  MYKK.
Tumeelezea ni kwa nini maambukizi haya yaitwe Mambukizi Yanayosambazwa  kwa Kujamiana na siyo Magonjwa Yanayosambazwa wa Kujamiana (STD) au Magonjwa ya Sinaa. Tuyaite Maambukizi Yanayosambazwa kwa Kujamiana au kwa kizungu STI. Wiki ujayo tutataja na kuanza kuelezea aina 13 za MYKK

0 comments:

Post a Comment