Tuesday 26 November 2013

Zitto Ajiweka Njia panda CHADEMA..!!


Aliyekuwa Naibu Katibu Mkuu wa Chadema, Zitto Kabwe amejiweka katika mazingira magumu zaidi kisiasa ndani ya chama hicho, kutokana na shaka kubwa iliyougubika mkutano wake na waandishi wa habari uliofanyika Dar es Salaam juzi.
  

Zitto pamoja na viongozi wengine wawili wa Chadema; Dk Kitila Mkumbo na Samson Mwigamba walivuliwa nyadhifa zao na Kamati Kuu ya Chadema baada ya kubainika kupanga mbinu za uasi, kupitia waraka ambao ulikuwa ukieleza mkakati wa kufanya mabadiliko makubwa ya kiuongozi wakati wa uchaguzi mkuu wa ndani.
Leo, uongozi wa Chadema umeitisha mkutano wa waandishi wa habari ambao pamoja na mambo mengine, utajibu baadhi ya hoja za utetezi ambazo zilitolewa na Zitto pamoja na Dk Kitila. Katika mkutano wa juzi, Zitto na Dk Kitila ambaye alikuwa Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chadema, walizungumzia kuvuliwa kwao madaraka, lakini maandalizi na uendeshaji wa mkutano huo yanazua shaka kutokana kuwahusisha watu wanaodaiwa kuwa ni wanachama wa Jumuiya ya Vijana ya Chama cha Mapinduzi (UVCCM).
Miongoni mwao, wamo waliowahi kuwa wanachama wa Baraza la Vijana la Chadema (Bavicha), Habib Mchange na Mtela Mwampamba ambao walitimuliwa kwa makosa yanayofanana na yale yalizosababisha Zitto na wenzake kuvuliwa nyadhifa zao.
Mchange na Mwampamba pamoja na aliyekuwa Makamu Mwenyekiti wa Bavicha, Juliana Shonza, walivuliwa uanachama wa Baraza hilo Januari 5, mwaka huu baada ya kupatikana na hatia ya kutumia mitandao ya kijamii kukihujumu Chadema na kuwatukana viongozi wake wakuu. Baadaye walihamia CCM wanakoendeleza harakati zao za kisiasa.
Jana, Machange alipotafutwa, alisema: “Mimi sikuwahi kuondoka Chadema, nilifukuzwa kihuni kama walivyowafanyia Zitto na Kitila. Nimepeleka malalamiko yangu tangu Januari hadi leo sijajibiwa, hivyo siwezi kusema nimeondoka.
Nataka nimuunge mkono mwathirika mwenzangu kama ilivyokuwa mimi lakini nitabakia kuwa mwanachama mwaminifu.
“Mimi ni mwanaChadema na sikuwahi kujiunga na CCM au chama chochote, walioondoka ni Mwampamba na Shonza.” Mwampamba alisema: “Nilijitokeza pale kuonyesha mshikamano kwa sababu mimi pia ni mwathirika. Kwa hiyo nilitaka ulimwengu ufahamu kuwa mimi ni kati ya wanaopinga siasa za aina hii... Chadema ni chama kinachojiandaa kuchukua dola, sasa kama kila mwenye mawazo tofauti anaonekana mhaini itakuwaje siku wakichukua dola? Ubaguzi huu haujalishi uko chama gani, hata kama niko CCM, hilo halinizuii kuungana na mtu aliyepatwa na tatizo kama langu.”
Kuwepo kwao katika mkutano wa Zitto kunaweza kutumiwa na uongozi wa Chadema kuwa uthibitisho wa kiongozi huyo kushiriki katika uasi na kunaweza kupuunguzia nguvu utetezi unaotolewa na Dk Kitila kwamba hakuwa sehemu mpango wa kuuondoa uongozi wa sasa madarakani. Zitto, Dk Mkumbo na aliyekuwa Mwenyekiti wa Chadema Mkoa wa Arusha, Samson Mwigamba wanasubiri kukabidhiwa barua za kuvuliwa kwao madaraka na katika siku 14 wanapaswa wawe wamewasilisha utetezi wao wakieleza kwa nini wasifukuzwe uanachama kutokana na tuhuma zinazowakabili.
Dk Slaa
Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Wilbrod Slaa alisema jana kuwa ilikuwa lazima viongozi hao wavuliwe madaraka hasa baada ya Dk Kitila kukiri kuhusika na waraka ambao anasema ulilenga kushinda kupitia uchaguzi halali ndani ya chama hicho.

“Hata katika ya nchi ukihusika kutengeneza mbinu za siri lazima ushughulikiwe.Hakuna Katiba itakayokuruhusu kufanya mipango ya siri. Kwanza uchaguzi wa Chadema nani katangaza mpaka mipango ianzwe kutengenezwa sasa hivi?” alihoji Dk Slaa.

 -----Mwananchi


0 comments:

Post a Comment