Friday 15 November 2013

KAGAME AHOFIA KUKIMBIWA EAC

Kufuatia Rais Yoweri Kaguta Museveni kuongea kwa kumaanisha kumtaka Rais wa Rwanda Paul Kagame kukaa meza moja na watu wanaompinga walioko DRC, Kagame alilazimika kuitisha mkutano wa dharura na washauri wake wakuu na kuwaeleza walichozungumza na Museveni. Katika maongezi yake, kwa mujibu wa taarifa zilizotoka kwa mmoja wa washauri hao Kagame alisema “nimekuwa nikiwaambia mara kwa mara kuwa tuko peke yetu. Hata Yoweri, tuliyemwamini kama rafiki yetu na mwenzetu anatugeuka! Leo anatuambia hiki, kesho anakwenda kukutana na viongozi wengine na kutubadilikia.”
Baadaye akawataka washauri hao kuja na mpango mkakati wa nini cha kufanya wakati huu Rwanda ikizidi kutengwa na nchi za Afrika na hata za nje ya Afrika.
Kwa mujibu wa mtandao wa AfroAmerica Network, Museveni, baada ya kurejea kutoka kwenye mkutano wa wakuu wa nchi za SADC na zile za Maziwa Makuu (IGGLR) huko Pretoria, Afrika Kusini wiki iliyopita, alimpigia simu Kagame na kumwambia: “Huenda sasa ni wakati muafaka wa kuzungumza na wapinzani wako wenye silaha.”
kagame Mwanzoni mwa mwezi, Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani, John Kerry na mwenzake wa Uingereza walimwonya Kagame kuachana mara moja na ushiriki wake kwenye machafuko ya mashariki mwa DRC, ikiwa ni mara ya pili ndani ya mwaka mmoja kwa wakubwa hao kutoa onyo kama hilo.
Wakati hayo yakiendelea, zipo taarifa kwamba Rais Museveni amepanga kutuma ujumbe nchini kuja kuzungumzia mustakabali wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) baada ya Rais Jakaya Kikwete kuwaambia Watanzania kwamba Tanzania haijakiuka chochote katika makubaliano ya msingi, ila wenzetu hao ndio huenda wana ajenda yao.
Kauli ya Kikwete ilihitimisha hali ya wasiwasi wa Tanzania kujitoa EAC na iwapo ujumbe wa Uganda utakuja, itakuwa ni mwendelezo wa kilichofanywa mwishoni mwa wiki na Kenya waliomtuma Waziri wa Mambo ya Nje kuja Dar es Salaam kuweka mambo sawa.

0 comments:

Post a Comment