Saturday 16 November 2013

ZITO APEWA ULINZI

JESHI la Polisi limempa ulinzi wa siri Mbunge wa Kigoma Kaskazini,Zitto Kabwe (CHADEMA) kama njia ya kumkinga asidhuriwe na maadui wake katika siasa.
Hatua hiyo ya polisi imechukuliwa siku chache baada ya mwanasiasa huyo kijana na mama yake mzazi, Shida Salum, kwa nyakati tofauti, kudai kuwa Zitto amekuwa akiwindwa na watu ambao wamekuwa wakitishia uhai wa wake kutokana na siasa zinazoendelea ndani ya Chadema.
Chanzo cha kuaminika kutoka ndani ya Jeshi la Polisi, kiliiambia RAI kuwa uamuzi huo ulifikiwa katika kikao wiki iliyopita, baada ya jeshi hilo kupata taarifa za tishio la kudhuriwa kwa kiongozi huyo kwa kile kilichoelezwa kuwa tofauti baina yake na viongozi wenzake wa Chadema.
Kikao hicho ambacho kiliwahusisha makamishna kutoka makao makuu ya jeshi hilo, kilipitia kwa kina taarifa ya kutaka kudhuriwa kwa Zitto kwa kutofautiana msimamo na viongozi wenzake ndani ya chama hicho.
“Kikao kilifanyika Novemba 11 mwaka huu ambako pamoja na mambo mengine kimeweza kujadili kwa kina kutaka kudhuriwa Zitto … hivyo walitumwa makachero wa jeshi la polisi waweze kubaini anapoishi.
zkabwe
“Wamefanya kazi hii na sasa kiongozi huyo analindwa kuanzia nyumbani kwake Tabata. Askari maalumu wamepewa kazi ya kuimarisha ulinzi nyumbani kwake hadi katika nyendo zake,” kilisema chanzo hicho ndani ya jeshi la polisi.
Zitto, ambaye pia ni Naibu Katibu Mkuu wa Chadema, kwa muda mrefu amekuwa akitofautiana na viongozi wenzake hasa katika masuala ya taifa hali inayofanya atafsiriwe kuwa anatumika kutaka kuivuruga Chadema.
RAI ilimtafuta Msemaji wa Jeshi la Polisi Tanzania, Advera Senso kupata uthibitisho wa uamuzi huo lakini alisema suala hilo liko mikononi mwa Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Suleiman Kova.
“Kwa jambo hili nakuomba mtafute Kamanda wa Mkoa husika, yeye anaweza kukupa maelezo ya kina ya jambo hilo ndugu yangu au Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam,” alisema Senso.
KOVA
Alipotafutwa jana, Kova alisema hawezi kukubali au kukata kwa sababu suala hilo liko katika mamlaka ya Kamanda wa Polisi Mkoa wa Ilala, Marietha Minangi.
“Siwezi kusema ndiyo au hapana, nakuomba umtafute kamanda wa mkoa husika atakupatia maelezo ya kina,”alisema Kamanda Kova.
KAMANDA WA ILALA
Kamanda Minangi alipoulizwa jana kuhusiana na suala hilo, naye alimrushia mpira Kova akisema ndiye pekee anayeweza kutoa ufafanuzi wa suala hilo.
“Jamani nawaomba suala hili mmtafute Kamanda Kova ndiye anayeweza kulitolea ufafanuzi,”alisema Kamanda Minangi.
Kwa muda mrefu sasa, Zitto amekuwa akishutumiwa na viongozi wenzake wa ngazi za juu katika Chadema akidaiwa kutengeneza ufa baina yake na wazito ndani ya chama hicho tangu mwaka 2009.
Zitto amekwisha kuwahi kutangaza uamuzi wa kutaka kuwania uenyekiti wa chama hicho aweze kupambana na mwenyekiti wake, Freeman Mbowe.
Hata hivyo baadaye alijiondoa kuwania nafasi hiyo baada ya wazee wa chama hicho kuingilia kati na kumsihi atumie busara kutogombea.
Katika siku za hivi karibuni, Zitto amejikuta akihusishwa na kile kinachotajwa kuwa nyuma ya `usaliti’ unaodaiwa kufanywa na Mwenyekiti wa Chadema Mkoa wa Arusha aliyesimamishwa, Samson Mwigamba.
Hata hivyo, Zitto alikanusha tuhuma hizo na kuwataka viongozi wenzake kuelekeza nguvu kwa wanachama akisema malumbano hayatakijenga chama.
Mbali na hilo, kwa muda mrefu Zitto amekuwa na msuguano wa ndani na nje ya chama, hasa kutokana na misimamo yake.
Hivi karibuni, Mbunge Arusha Godbless Lema (Chadema) aliibuka na kumtuhumu Zitto kwa uamuzi wake wa kutochukua posho za vikao bungeni tofauti na msimamo alioutoa mwaka 2011.
Msuguano mwingine ni baina yake na vyama vya siasa kwa msimamo wake wa kutaka vyama vyenye wabunge ambavyo vinapata ruzuku ya serikali, viwasilishe ripoti ya ukaguzi wa hesabu zake kwa Msajili wa Vyama vya Siasa.
Zitto ambaye ni mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) pia aliwaonya viongozi wenzake kuacha propaganda kwa kulichukulia suala hilo kuwa ni la siasa au lake binafsi.
Alisema anachokifanya ni kusimamia sheria kutokana na nafasi yake kama mwenyekiti wa PAC.
Vyama vya siasa vinatajwa kuchukua ruzuku ya Sh bilioni 67.7, lakini havijaanika mchanganuo wa matumizi yake.
ATUA POLISI
Katika hatua nyingine, jana Zitto alisambaza ujumbe kwenye mtandao wake wa jamii akisema amelazimka kwenda makao makuu ya jeshi la polisi kutoa maelezo kwa kutishiwa kifo.
Katika ujumbe huo alindika: “Nimetoka makao makuu ya upelelezi kuandika maelezo kuhusu vitisho dhidi yangu, kufuatia hekaya inayoitwa ripoti ya siri ya Zitto Kabwe.
“Chanzo cha hekaya ya sasa kinabadilishwa kutoka makao makuu ya Chadema na kuwa ni Usalama wa Taifa au Chama Cha Mapinduzi (CCM)”.
Taarifa hiyo ilisema wahusika wanaendelea kuhamisha chanzo, lakini wanaopaswa kujua watasakwa, kukamatwa na kuburuzwa mahakamani.
“Nimewashtaki kwa kunitishia maisha, ninawashtaki kwa kunichafua kwa tuhuma za uongo, nafanya haya kwa lengo la kuhakikisha siasa za kuzushiana na kusambaza uongo zinakuwa na gharama kubwa,”ilisema taarifa hiyo.
MSIMAMO WAKE
Mwanasiasa huyo kijana ambaye amejipambanua kuwa mtetezi wa misingi ya utaifa, raslimali za nchi, uchumi na masuala ya utawala bora ndani na nje ya chama chake, alitoa msimamo wake kwa mara ya kwanza wiki iliyopita alipohutubia mkutano mkubwa wa hadhara katika uwanja wa Kolimba wilayani Kaliua, Mkoa wa Tabora.
“Katika umri huu mdogo, nimepigwa mishale mingi ya siasa, mimi ni binadamu nina damu, nikipigwa hii mishale damu inatoka, ninaumia, sasa nimechoka kupigwa mishale, lazima sasa tuambiane ukweli,” alisema Zitto.
Saa kadhaa baada ya hotuba yake hiyo, alisambaza tamko la maandishi ambalo lilibeba ujumbe unaofanana na ule alioutoa Kaliua.
Awali katika mkutano wa Kaliua, Zitto alisema alikuwa hayuko tayari kuendelea kukaa kimya pasipo kuchukua hatua zikiwamo za sheria wakati akichafuliwa.
Alisema alikuwa ameshamwandikia barua Katibu Mkuu wake, Dk. Willbrod Slaa akihoji iwapo taarifa ya kumchafua iliyosambazwa katika mitandao ya intaneti chini ya kichwa cha habari kisemacho, “Taarifa ya Siri ya Chadema” ni ya chama hicho au la.
Zitto aliyekuwa akizungumzia matokeo ya ziara yake ya kufuatilia fedha zilizofichwa na baadhi ya Watanzania katika benki za Uswisi na kwingineko Ulaya, alieleza kusikitishwa na kile alichodai kuwa ni kikundi cha watu ndani ya Chadema ambacho kimekuwa mstari wa mbele kumpaka matope.
“Wakati nafanya kazi hii ya hatari ya kufuatilia hizo fedha zilizofichwa nje ya nchi, navunjwa nguvu na watu ambao tuko chama kimoja kwani imekuwa ni kawaida unapofanya siasa, lazima upate mashambulio na sasa nashambuliwa na chama changu.
“Katika hali ya kawaida, wenzagu tulionao katika chama ndiyo waliopaswa kunipa nguvu kwa vile tuna kazi kubwa ya kupambana na ‘lidude likubwa linaloitwa CCM,” alisema Zitto.
Bila kutaja jina la mtu, alisema kuna watu wachache ambao hawana kazi ndani ya chama hicho ambao shughuli yao imekuwa ni kugonganisha viongozi wagombane.
Akirejea historia ya kuchafuliwa kwake, Zitto alisema hali hiyo ilianza mwaka 2009 baada ya kujitokeza kutaka kugombea uenyekiti wa Chadema akichuana na Freeman Mbowe.
Chanzo: Mtanzania

Alisema alikuwa ameshamwandikia barua Katibu Mkuu wake, Dk. Willbrod Slaa akihoji iwapo taarifa ya kumchafua iliyosambazwa katika mitandao ya intaneti chini ya kichwa cha habari kisemacho, “Taarifa ya Siri ya Chadema” ni ya chama hicho au la.
Zitto aliyekuwa akizungumzia matokeo ya ziara yake ya kufuatilia fedha zilizofichwa na baadhi ya Watanzania katika benki za Uswisi na kwingineko Ulaya, alieleza kusikitishwa na kile alichodai kuwa ni kikundi cha watu ndani ya Chadema ambacho kimekuwa mstari wa mbele kumpaka matope.
“Wakati nafanya kazi hii ya hatari ya kufuatilia hizo fedha zilizofichwa nje ya nchi, navunjwa nguvu na watu ambao tuko chama kimoja kwani imekuwa ni kawaida unapofanya siasa, lazima upate mashambulio na sasa nashambuliwa na chama changu.
“Katika hali ya kawaida, wenzagu tulionao katika chama ndiyo waliopaswa kunipa nguvu kwa vile tuna kazi kubwa ya kupambana na ‘lidude likubwa linaloitwa CCM,” alisema Zitto.
Bila kutaja jina la mtu, alisema kuna watu wachache ambao hawana kazi ndani ya chama hicho ambao shughuli yao imekuwa ni kugonganisha viongozi wagombane.
Akirejea historia ya kuchafuliwa kwake, Zitto alisema hali hiyo ilianza mwaka 2009 baada ya kujitokeza kutaka kugombea uenyekiti wa Chadema akichuana na Freeman Mbowe

0 comments:

Post a Comment